We mnyang'anyi jameni

by JackSwaleh , August 15, 2024

We mnyang'anyi jameni, sasa mbona hivi kweli
Nasema nawe mhuni, waona hii halali?
Nimechumia juani, usiku pia silali
Sasa hapo kivulini, wakula ya kwangu mali

Wazunguka na kiburi, kwangu chungu na machozi.
Mjini sasa ni pori, hayawani we jambazi
Yanizidi sana mori, wanizidia ujuzi
Nitajua yako siri, wizi nayo sio kazi

Itawa telezi miti, njia tu zitafungika
Utafikia tamati, itawa finyu mipaka
Kuishi nayo bahati, yako nayo tutapoka
Ukipoteza sijuti, kulaani sitachoka

Unaeza penda kusoma: "Subira Yaniumiza"